HIVI NDIVYO POLISI WALIVYOUAWA KATIKA TUKIO LA UVAMIZI KITUONI IKWIRIRI - MAISHA ONLINE BLOG

Hot

Post Top Ad

Your Ad Spot

Thursday, January 22, 2015

HIVI NDIVYO POLISI WALIVYOUAWA KATIKA TUKIO LA UVAMIZI KITUONI IKWIRIRI

ASKARI wawili wa Jeshi la Polisi katika Kituo cha Ikwiriri wilayani Rufiji mkoani Pwani, wameuawa baada ya kushambuliwa kwa silaha na majambazi, waliovamia kituo hicho na kuiba silaha baada ya kufanikisha mauaji.
Kutokana na tukio hilo, Jeshi la Polisi liko katika msako mkali, huku Mkuu wa jeshi hilo, IGP, Ernest Mangu akitangaza donge nono la Sh milioni 20 kwa watakaofanikisha kukamatwa kwa wahusika wa tukio hilo na silaha.
Akizungumza na waandishi wa habari kwa njia ya simu kutoka eneo la tukio, Ikwiriri, Kamanda wa Polisi mkoani Pwani, Ulrich Matei alisema majambazi hao walitumia silaha kuwaua askari hao.
Kamanda Matei alisema kuwa tukio hilo lilitokea majira ya saa 8 usiku katika kituo hicho cha Polisi cha Ikwiriri.
 Aliwataja askari waliokufa kuwa ni mwenye namba E 8732 Koplo Edgar Milinga na WP 5558 Konstebo Judith Timothy.
Alisema licha ya kufanya mauaji hayo, pia majambazi hao yalipora silaha tano za moto aina mbalimbali, zikiwemo SMG 2, SAR 3 na risasi 60. Pia, walichukua mabomu mawili ya machozi.
Kamanda alisema kuwa pia watu hao, waliharibu kwa kulipiga risasi gari la Polisi la kituo hicho lenye namba za usajili PT 1965.
Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini, Advera Bulimba alisema tukio hilo la kusikitisha, halitapita hivi hivi, bali jeshi limeelekeza nguvu zake huko kuhakikisha wahusika wanakamatwa.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot